Jumapili, 2 Julai 2017

SWALA YA IJUMAA

Sala ya Ijumaa
Imeitwa Sala ya Ijumaa kwa vile inasaliwa siku ya Ijumaa, au kwa yale ya kheri yaliomo kwenye siku hii. Sala ya Ijumaa ni bora yao ya Sala na siku ya Ijumaa ni bora yao ya siku. Hivi ni kwa qauli ya Mtume  s.a.w.:

"Bora ya siku zilizochomoza jua juu yake ni siku ya Ijumaa, siku hio ameumbwa Adam a.s., na siku hio ametiwa Peponi, na siku hio ametoka Peponi, wala hakitasimama Qiyama isipokuwa siku ya Ijumaa". (Imehadithiwa na Muslim na Abu Daud na Al Nissaai na Al Tirmidhy).
Hukmu Yake
Sala ya Ijumaa ni waajibu kwa Qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, qauli ya Mtume s.a.w. na itifaqi ya wanazuoni. Ametwambia Mwenyezi Mungu Mtukufu:
 "Enyi mlio amini! Ikiadhiniwa Sala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni biashara ……". (Al Jumu'a : 9).
Na amesema Mtume s.a.w.:


"Niliazimia nimuamrishe mtu asalishe, kisha nende nikawachomee moto nyumba zao watu wasiokwenda kusali Sala ya Ijumaa ". (Imehadithiwa na Muslim).
Na katika upokezi mwengine:

"Wasiwache watu kutekeleza Sala ya Ijumaa, wakiwacha Mwenyezi Mungu atapiga mihuri kwenye nyoyo zao na hapo watakuwa miongoni mwa walioghafilika". (Imehadithiwa na Muslim na wengineo).
Na Hadithi nyengine ya Matume s.a.w.:      "Kuiendea Sala ya Ijumaa ni waajibu kwa kila balegh". (Imehadithiwa na Al Nissaai).
Na Hadithi nyengine ya Mtume s.a.w.:
   "Mwenye kuwacha kusali Sala ya Ijumaa, Ijumaa tatu (mfululizo); Mwenyezi Mungu hupiga muhuri kwenye moyo wake". (Imehadithiwa na Abu Daud na Al Tirmidhy na Al Nissaai).
Shuruti za Kuwajibikia Sala ya Ijumaa
Shuruti za kuwajibikia Sala ya Ijumaa ni saba:
Ya Kwanza, Uislam, kama ilivyotajwa kwenye Kitabu cha Sala.
Ya Pili mpaka ya Sita, kuwa huru, baalegh, mwenye akili kamilifu, mwanamume, mzima wa siha. Hivi ni kwa qauli ya Mtume  s.a.w.:
"Sala ya Ijumaa ni waajibu kwa kila Muislam, isipokua kwa watu wanne, mwenye kumilikiwa, mwanamke, mtoto mdogo na mgonjwa". (Imehadithiwa na Abu Daud).
Mgonjwa wa akili yeye si mwenye kukalifishwa na Sharia kwa lolote lile. Kwenye hukmu ya ugonjwa imekisiwa kuingia, kukosa cha kusitiri utupu, kukhofu dhulma na madhaalim, na mwenye tumbo la kuendesha na hawezi kujizuia; lau itakhofiwa maiti kuharibika, watu wataacha kwenda
kusali Sala ya Ijumaa na kumshughulikia maiti mpaka kumzika.
Ya Saba, mkaazi, si msafiri; haimuwajibikii Sala ya Ijumaa msafiri. Hivi ni kwa vile haikupokewa kuwa Mtume s.a.w. amewahi kusali Sala ya Ijumaa nae yumo safarini, bali imepokewa kuwa:   "Haimlazimu Sala ya Ijumaa aliomo safarini". (Imehadithiwa na Al Bayhaqy).
Shuruti za Kusihi Sala ya Ijumaa
Mbali na shuruti za Sala tulizotangulia kuzitaja, kusihi Sala ya Ijumaa ina shuruti tatu ziada:
Ya Kwanza, iwe kwenye pahala wanapoishi idadi ya watu wenye kutimiza Sala ya jama'a, kwa aina yoyote ile ya majengo.
Ya Pili, isaliwe jama'a; haikuwahi kupokewa kwamba Mtume wetu Mpezni s.a.w. au Makhalifa wa baada yake wamewahi kusali Sala ya Ijumaa mtu peke yake. Idadi ya watu wenye kufanya jama'a ya kulazim Sala ya Ijumaa wasipungue watu arubaini. Kwa Hadithi ya Jaabir r.a. kwamba:
    "Imekuwa ni mwenendo kwamba kila penye watu arubaini na zaidi (husaliwa) Sala ya Ijumaa". Imehadithiwa na Al Bayhaqy).
Na kwa Hadithi ya Ka'ab bin Malik r.a.:
 "Mtu wa mwanzo kutusalisha Sala ya Ijumaa kwenye kijiji cha Khudhamaat ni As'ad bin Zaraara na tulikuwa watu arubaini". (Ibnu Hibbaan na Al Bayhaqy waimeipa darja ya Hadithi sahih).
Na kwa Hadithi nyengine kwamba Mtume s.a.w.:
  "Mtume s.a.w. amesali Sala ya Ijumaa akiweko Madina, wala haikupokewa kutoka kwake kwamba alisali Sala ya Ijumaa kwa uchache ya watu arubaini".
Ya Tatu, isaliwe kwenye wakati wake, wakati wake ni ule wakati wa Sala ya adhuhuri. Hivi ni kwa qauli ya Anas r.a.:
    "Mtume s.a.w. alikuwa akisali Sala ya Ijumaa baada ya kutenguka jua". (Imehadithiwa na Al Bukhary).
Imepokewa kutoka kwa Salama bin Al Aku'i r.a.:
 "Tulikuwa tukisali Sala ya Ijumaa pamoja na Mtume s.a.w. linapotenguka jua".
Ikiwa itakuwa dhiki ya wakati, ikawa haiwezekani kusaliwa Sala ya Ijumaa, basi itasaliwa Sala ya adhuhuri badala ya Sala ya Ijumaa. Ikiwa wataingiwa na shaka kama wakati umetoka au laa, basi watasali Sala ya adhuhuri, kwani kuhakikisha kuweko wakati ni sharti ya kusihi Sala.
Fardhi za Sala ya Ijumaa
Fardhi za Sala ya Ijumaa ni tatu:
Ya Kwanza, itanguliwe na khutba mbili, baina ya khutba na khutba kitako. Imepokewa kutoka kwa Jaabir bin Samra r.a. kwamba Mtume s.a.w.:
 "Mtume s.a.w. alikuwa akikhutubu khutba mbili na akikaa baina ya khutba mbili hizo, na akikhutubu hali amesimama".
Imepokewa vile vile:
  "Hakika ya Mtume s.a.w. alikuwa akikhutubu khutba mbili, akisoma Qur'ani na akiwaadhi watu".
Nguzo za Khutba ya Ijumaa
Khutba ya Sala ya Ijumaa ina nguzo tano:
Kwanza, kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Pili, kumsalia na kumuombea Rehma Mtume s.a.w.
Tatu, kuusia watu kumcha Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Nne, kuwaombea du'a Waumini kwenye khutba ya pili.
Tano, kusoma Qur'ani; uchache wake ni Aya kaamili.
Shuruti za Khutba ya Sala ya Ijumaa
Khutba ya Sala ya Ijumaa ina shuruti saba:
Kwanza, kuingia wakati wa Sala.
Pili, kutangulia khutba mbili kabla ya Sala.
Tatu, kusimama; kwa mwenye kuweza.
Nne, kukaa kitako baina ya khutba mbili kwa kiasi cha kutulia.
Tano, ku'tahirika na hadathi kubwa na ndogo na najsi (uchafu), mwilini, nguoni, na mahala pakusalia.
Sita, kusitiri utupu kwa nguo ilio 'taahir.
Saba, kutoa sauti ya kusikilika na watu arubaini ambao wanalazimika na hii Sala.
Fardhi ya Pili, isaliwe raka'a mbili; hivi ni kwa qauli ya Sayyidna 'Umar r.a.:
  Maana yake ni kama hivi: "Sala ya Ijumaa ni raka'a mbili bila ya kupunguza, kama alivyosema Mtume s.a.w.".
Fardhi ya Tatu, isaliwe jama'a; tumeshataja dalili ya hivi.
Haiati (Mapambo) ya Sala ya Ijumaa
Inasuniwa kwa mwenye kwenda kusali Sala ya Ijumaa, mambo manne:
La Kwanza, akoge, hivi ni kwa qauli ya Mtume s.a.w.:
  "Mwenye kwenda kusali Sala ya Ijumaa basi naakoge". (Imehadithiwa na Al Sheikhan).
La Pili, asafishe kiwiliwili chake uchafu wenye kusababisha harufu mbovu ya mwili, na hivyo ndivyo inavyokusudiwa kwa kusemwa akoge, sio basi ajimwagie maji. Amesema Imam Shafi'ii r.a.:

"Mwenye kunadhifisha nguo zake hupungua wasiwasi wake, na mwenye kufanya harufu yake kuwa nzuri (kujitia manukato) huzidi akili yake".
La Tatu, kujipamba kwa kuvaa nguo nzuri na kwa kujitia manukato. Hivi ni kwa qauli yake Mtume s.a.w.:
"Mwenye kukoga siku ya Ijumaa na akavaa nzuri mno ya nguo zake na akajitia manukato kutoka nyumbani kwake - ikiwa anayo - kisha akenda kusali Ijumaa, akiingia msikitini asikiuke watu waliokwishakaa (kutaka kwenda mbele), kisha akasali alicho andikiwa, kisha akamsikiliza imam, mpaka akamaliza Sala yake; huwa ni kafara kwake kwa kiliopo baina ya Ijumaa hii na Ijumaa iliopita".  (Imepokewa na Ibnu Hibban na Al Haakim).
Kuvaa nguo nyeupe kwa kuhudhuria Sala ya Ijumaa ni bora zaidi. Hivi kwa qauli ya Mtume s.a.w.:
  "Vaeni nguo nyeupe, kwani hizo ni bora mno ya nguo zenu; na kwa nguo nyeupe wakafinini maiti wenu".
La Nne, kukata kucha na nywele zenye kupendeza kuondolewa; kwani hivi ni katika unadhifu.
Kusikiliza Khutba na Khilafu Ziliopo
Wamekhitalifiana rai wanazuoni juu ya hukmu ya kuzungumza wakati wa khutba ya Sala ya Ijumaa. Amesema Imam Shafi'ii r.a. na Imam Malik na Imam Abu Hanifa r.a. na Imam Ahmad r.a. kwamba inaharimishwa kuzungumza wakati wa khutba ya Sala ya Ijumaa. Wao wametolea hoja Qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
  "Na isomwapo Qur'ani isikilizeni na mnyamaze ili mupate kurehemiwa". (Al AĆ”raaf: 204).
Wamesema wengi wa wafasiri wa Qur'ani kwamba Aya hii imeteremshwa kukhusu khutba ya Sala ya Ijumaa. Na imeitwa hii khutba kwa jina la Qur'ani kwa vile imo ndani yake Qur'ani Tukufu. Na qauli ya Mtume s.a.w.:
 " Ukisema kumwambia sahibu yako kwenye Sala ya Ijumaa na Imam anakhutubu - sikiliza - basi itakuwa umefanya kosa". (Imehadithiwa na wapokezi wa Hadithi isipokuwa Ibni Maajah).
Na rai nyengine ya Imam Shafi'ii r.a. ni kwamba haiharimishwi kusema, bali kusikiliza ni sunna kama walivyopokea Al Sheikhan kuwa Sayyidna 'Uthman r.a aliingia msikitini siku ya Ijumaa na Sayyidna 'Umar r.a. anakhutubia, akasema Sayyidna 'Umar r.a. kumwambia Sayyidna 'Uthman r.a.: "Nini hali ya watu wanataakhari kuitikia wito? Akasema Sayyidna 'Uthaman r.a.: Yaa Amir-l-Muuminiin! Baada ya kusikia adhana, nimetia udhu na nikaja msikitini". Na imehadithiwa kuwa wakati Mtume s.a.w. yuko juu ya membari anakhutubia siku ya Ijumaa aliingia mtu na kuuliza kwa kelele: "Lini Qiyama"? Watu wakamuashiria anyamaze, lakini hakufanya hivyo. Na akarejea na maneno yake, baada ya dakika Mtume s.a.w. akasema kumwambia: "Na uwe pole, umekiandalia nini? Akasema yule mtu: "Mapenzi ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake". Akasema s.a.w.: "Hakika yako wewe na unaempenda". ( Imehadithiwa na Al Bayhaqy ).
Hoja ya kwamba kusema wakati wa khutba si haraam ni vile kuwa Sayyidna 'Uthman r.a. alisema kwa kumjibu Sayyidna 'Umar r.a., na kwamba Mtume s.a.w. hakumkanya yule alieuliza lini Qiyama, na lau kama ni haraam basi angalimkanya kusema. Hii khilafu iliopo kukhusu kusema au kutosema haikhusiani na kitu muhim na cha dharura, katika hali hio haikatazwi kusema; bali ni waajibu kusema; kama vile kumuongoza kipofu, au kuona mtu anatambaliwa na nnge ukamzindua, au kumuona dhaalim amemuandama mtu ukamtanabahisha, au kuamrisha mema na kukataza maovu.
Kujuzu Kusali wakati Imam Anakhutubu
Wamekhitalifiana rai wanazuoni juu ya kwamba mtu akiingia msikitini siku ya Ijumaa na Imam anakhutubu, inajuzu asali raka'a mbili za tahiyatu-l-masjid au asisali. Wamesema baadhi ya wanazuoni kuwa asisali, na imepokewa hivi kutoka kwa Ibni 'Umar r.a., na Sayyidna 'Uthman r.a. na Sayyidna 'Ali r.a.; na kwa hii amri ya kusikiliza. Wakatoa dalili juu ya kisa cha Saliik r.a. kwamba alikuwa hana nguo, Mtume  s.a.w. akamuamrisha asimame ili watu wamuone wampe sadaqa. Amesema Imam Shafi'ii r.a. na Ahmad na Is-haaq na wanazuoni wakisasa wengine kuwa inapendekezwa asali tahiyatu-lmasjid raka'a mbili fupi kabla ya kukaa, wao wametolea hoja hivi kwa qauli ya Mtume s.a.w. juu ya Saliik wakati alipoingia msikitini akakaa kitako na Mtume s.a.w. anakhutubia kwenye Sala ya Ijumaa, Mtume s.a.w. alimuuliza Saliik: "Umesali ewe fulani? Akajibu: "Laa", yaani si kusali; Mtume  s.a.w. akamwambia: , yaani inuka uruku'i, yaani usali. Na katika upokezi mwengine:  yaani inuka usali raka'a mbili. Na katika upokezi mwengine:  yaani sali raka'a mbili. Na katika upokezi mwengine:
  "Akiingia mmoja wenu msikitini siku ya Ijumaa na Imam anakhutubu, basi naasali raka'a mbili". Na katika upokezi mwengine:
 ""  "……., na Imam anakhutubia, naaruku'i raka'a mbili, na azifupishe".
Hadithi zote hizi zimo kwenye Kitabu cha Hadithi cha Imam Muslim r.a. na zimetaja wazi kupendeza kusali raka'a mbili khafifu za   (kuamkia msikiti) unapoingia msikitini siku ya Ijumaa na Imam anakhutubu. Hivi ni kwa mwenye kuingia msikitini na Imam ana khutubu. Ama yule aliyomo msikitini tangu kabla ya Imam kuanza khutba, na akainuka kusali wakati Imam anakhutubu, hivi haijuzu; hata ikiwa kwa raka'a khafifu.
Kusoma Surat Al-Kahfi
Inasuniwa kusoma Surat Al-Kahfi, usiku wa kuamkia Ijumaa (Alkhamis usiku kuamkia Ijumaa), au Ijumaa yenyewe. Kusoma Surat Al-Kahfi mchana wa Ijumaa kumekuja kwa qauli ya Mtume s.a.w:

 "Mwenye kusoma Surat Al-Kahfi siku ya Ijumaa hun'garishiwa nuru baina ya Ijumaa na Ijumaa". (Imehadithiwa na Al Haakim na Al Bayhaqy).
Kusoma Surat Al-Kahfi usiku wa kuamkia Ijumaa kumekuja kwa qauli ya Mtume s.a.w:
"Mwenye kuisoma (yaani Surat Al-Kahfi) usiku wa kuamkia Ijumaa hun'garishiwa nuru (yenye kuenea) baina yake na baina ya Bait-l-'atiiq (Msikiti wa Makka)". (Imehadithiwa na Al Bayhaqy).
Ni waajibu mtu anaposoma Qur'ani - Surat Al-Kahfi - au Sura nyengine yoyote ile, iwe si kwa kumghasi au kumshawishi mwenzake anaesoma, au anaesali au mwenye kuvuta uradi; kwa vile yeye kusoma kwa sauti ya kughasi. Kufanya hivyo ni haraam, amesema Mtume  s.a.w. :

"Hakika kila mmoja wenu ni mwenye kusema na Mola wake Mlezi, basi musiudhiane, walaa asitoe sauti mmoja wenu wakati akisoma". Wakati bora wa kusoma Surat Al-Kahfi ni baada ya Sala ya alfajiri, kwa kukimbilia kheri. Ama vile wanavyofanya watu wengi, yaani kuisoma msikitini na kwa sauti ya kughasi wengine katika ibada zao, hivi haifai; bali imeharimishwa.

 MAREJEO