Jumatatu, 7 Agosti 2017

KUKUSANYWA NA KUHIFADHIWA KWA QURAN

Kukusanywa na Kuhifadhiwa kwa Qur’an.
§  Qur’an ina ahadi ya kuhifadhiwa na kulindwa na Mwenyezi Mungu (s.w) tofauti na vitabu vingine kama aya zifuatazo zinavyobainisha;
      “Hakika Sisi ndio tulioteremsha mawaidha haya (Qur’an) na hakika Sisi ndio tutakayoyalinda”  (15:9).
      “Hakitakifikia batili mbele yake wala nyuma yake, kimeteremshwa na Mwenye Hikima ahimidiwaye” (41:42).


§  Njia na Hatua zilizotumika katika kuihifadhi na kuilinda Qur’an.
Mtume (s.a.w) mwenyewe aliweka misingi madhubuti ya kuihifadhi na kuhakikisha kuwa Qur’an haipotei kupitia njia zifuatazo;

1.      Mtume (s.a.w) alihifadhishwa na kufanyishwa marejeo ya Qur’an yote na Malaika Jibril (a.s) mara kwa mara, hasa mwezi wa Ramadhani.
Rejea Qur’an (73:1-4), (2:185).

2.      Mtume (s.a.w) aliahidiwa kuwa atasomeshwa Qur’an na Mwenyezi Mungu (s.w) na hata sahau kamwe.
Rejea Qur’an (75:16-19) na (87:6-7).

3.      Mtume (s.a.w) aliwahifadhisha Maswahaba na Waislamu Qur’an vifuani mwao wakati ilipokuwa inashuka.
Zaidi bin Thaabit amesema: “…..kila nilipomaliza kuandika (Wahayi), Mtume (s.a.w) aliniamuru nisome nilichoandika na nilikuwa ninamsomea. Kama  palikuwa na kosa alilisahihisha kisha aliwapa watu (kunakili na kuhifadhi vifuani mwao)”.

4.      Maswahaba waliihifadhi na kuisoma Qur’an mara kwa mara hasa katika ibada za swala na zinginezo.
Rejea Qur’an (73:1-5).

5.      Mtume (s.a.w) aliwasomea waandishi wa Qur’an (wapatao 42) na kuandika kama walivyosomewa na kisha Mtume (s.a.w) aliwataka wasome ili ahakiki walichoandika.
Uthman bin Affan (r.a) amesimulia: “Wakati wowote Mtume wa Allah (s.a.w) alipoteremshiwa wahyi humuita mmoja wa watu waliochaguliwa kuandika.” (Ameipokea Tirmidh)”.

6.      Mtume (s.a.w) aliwaagiza na kuwasimamia waandishi wa Qur’an wapangilie sura na aya kama zilivyo katika msahafu akiongozwa na Malaika Jibril (a.s).
Uthman bin Affan (r.a) ameeleza: “Ilikuwa kawaida ya Mtume wa Allah kila iliposhuka aya za sura mbali mbali (za Qur’an) au kila aya iliposhuka alimuita mmoja wapo wa waandishi wa Qur’an na kumwambia, “andika aya hizi katika sura kadhaa baada ya aya kadhaa.”

§  Umihimu wa kunakiliwa upya Qur’an wakati wa Uthman bin Affan (r.a).
Khalifa Uthman bin Affan (r.a) aliteuwa waandishi 4 kunakili misahafu 7 kutoka kwenye msahafu ulioandikwa wakati wa Mtume (s.a.w) kwa sababu zifuatazo;

-     Kutokana na kupanuka Dola ya Kiislamu na kusambaa maswahaba na walimu wa Qur’an maeneo mbali mbali.

-     Kuwa na hitajio kubwa la kufundishwa ujumbe wa Qur’an sehemu mbali mbali hasa za ugenini.

-     Watu wengi waliingia katika Uislamu wakiwa wageni wa lugha ya Qur’an (Kiarabu) na kushindwa kuisoma na kupata ujumbe wa Qur’an.

-     Kuepusha kutofautiana kwa matamshi ya usomaji wa Qur’an ya asili katika ufikishaji wa ujumbe wa Qur’an.

-     Kuepusha kupatikana mwanya wa maadui wa Uislamu katika upotoshaji na upoteaji wa ujumbe wa asili wa Qur’an.